Monday, November 20, 2023

BINTI YETU



BINTI YETU










Ni heri basi arudi, kuliko kututesea,

Kwa sasa hatuna budi, sisi kama familia,

Hizo dhiki zimezidi, mrudishe twakwambia,

Binti yetu mrembo, huwezi kututesea

 

Kidato hakumaliza, kwa mimba ulompea,

Ukasema unaweza, mtoto kututunzia,

Nasi hatukukukataza, sharia tukafuatia,

Binti yetu mrembo, huwezi kututesea

 

Amehangaika sana, binti yetu malkia,

Si usiku si mchana, watoto kuwatafutia,

Kisa wewe memukana, hutaki kusaidia,

Binti yetu mrembo, huwezi kututesea

 

Hino ni simu ya saba, mtoto atupigia,

Kwa kesi za ukahaba, anazo kushtakia,

Japokuwa we ni baba, kwenye hio familia,

Binti yetu mrembo, huwezi kututesea

 

Anakukosea wapi, mpaka watutesea,

Binti yetu ni wa dini, na anaheshima pia,

Amefunzwa tamaduni, hana mambo ya dunia,

Binti yetu mrembo, huwezi kututesea

 

Wampiga kama fisi, hilo pia katwambia,

Tutahusisha polisi, ukome hizo tabia,

Ni heri aishi nasi, usije kutuulia,

Binti yetu mrembo, huwezi kututesea

 

Basi waite wazazi, muje kutuelezea,

Mambo yako yawe wazi, tuweze kusamehea,

La sivyo hatuwezi, binti kukurudishia,

Binti yetu mrembo, huwezi kututesea

 

Twashkuru mumefika, kesi kuifuatilia,

Kijana wenu hakika, binti ametutesea,

Kiapa kubadilika, wazazi tutaridhia,

Binti yetu mrembo, huwezi kututesea

Tuesday, October 10, 2023

KUMBUKUMBU



KUMBUKUMBU
 

Kilichofanyika kwangu, kimefunza hakika

Kuishi na walimwengu, ni utu na kadhalika,

Yote tumuachie Mungu, yatosha tulipofika,

Nina kumbukumbu nzuri, nina kumbukumbu mbaya.

 

Nikisha kusimulia, huruma tanionea,

Majina utanipea, Kwa yale nilopitia,

Nikweli sikusikia, ya baba alonambia,

Nina kumbukumbu nzuri, nina kumbukumbu mbaya.

 

Wema ulinitongea, nikajipata pabaya,

Kwa kweli sikudhania, yatanitokea haya,

Amini nilikusaidia, yote kumpatia,

Nina kumbukumbu nzuri, nina kumbukumbu mbaya.


Hadithi, hadithi njoo…Lakini hutoamini,

Tuache hadithi hio, sijui niseme nini,

Kidogo tena sikia, tuchambue jaladani,

Nina kumbukumbu nzuri, nina kumbukumbu mbaya.

 

Hua ni giza totoro, kile usichokijua,

Hakuonyesha kasoro, pale tulipoanzia,

Ningeina tumoro,Ruwa ningelikimbia,

Nina kumbukumbu nzuri, nina kumbukumbu mbaya.

 

Nimetamani kuchora, yote niloyapitia,

Yamejaa kwa fikira, yamejaa kwa hisia,

Mengine yananikera, mengine yanisumbua,

Nina kumbukumbu nzuri, nina kumbukumbu mbaya.

 

Nitachora siku moja, iwe kama ya filamu,

Kwa sasa, naomba, ngoja, tuitayarishe hamu,

Ili tunapoitaja, iwe tunaifahamu,

Nina kumbukumbu nzuri, nina kumbukumbu mbaya.

 

Duizo nimezikwepa, nakiri kutorudia,

Sirudii ninaapa, nitaishi kungojea,

Mola wangu atanipa, heri sasa kungojea

Nina kumbukumbu nzuri, nina kumbukumbu mbaya.


Green Ruwa

Mtoto Wa Gwiji 

 


Wednesday, June 8, 2022

MWAKA HUU SIKOPI

 


MWAKA HUU SIKOPI!

 

Kwanza Rabana asante, tarehe mosi mefika,

Yalopita sinikute, ya mwaka jana mashaka,

Lazima pesa nipate, kukopa nimeshachoka,

Mwaka huu sitakopa, e Mola nisaidie,

 

Nilikopa pasi utu, kuziba vyangu viraka,

Wakanilaumu watu, kwa kuwakopa haraka,

Naapa sitosubutu, kukukopa ewe kaka,

Mwaka huu sitakopa, e Mola nisaidie,

 

Shida zilikua nyingi, shingoni yalinifika,

Kukopa hio shilingi, sikupenda kwa hakika,

Mwaka huu pesa nyingi, walai ntazishika,

Mwaka huu sitakopa, e Mola nisaidie,

 

Wengine walinyamaza, kunipa hawakutaka,

Naapa nitajikaza, mambo haya kuepuka,

Si uongo yachukiza, kikosa kueleweka,

Mwaka huu sitakopa, e Mola nisaidie,

 

"Ukikopa kila mara, watakwita nyangarika"

Maneno haya hukera, lakini ya kweli kaka,

Yaweke kwenye fikira, usije kuabika,

Mwaka huu sitakopa, e Mola nisaidie,

 

Kwa wote nilowakopa, kina dada kina kaka,

Na wote walionipa, msaada nilotaka,

Shukrani ninawapa, nawaombea fanaka,

Mwaka huu sitakopa, e Mola nisaidie,

 

Kukopa mekuwa mwao, hawapendi kwa hakika,

Nimeona matokeo, vijana huhangaika,

Siseme shauri yao, wewe hayajakufika,

Mwaka huu sitakopa, e Mola nisaidie,

 

Wataftaji wenzangu, lazima *tutaomoka,

Shahidi shairi langu, mwenyewe nimeandika,

Riziki hugawa Mungu, tutapata bila shaka,

Mwaka huu sitakopa, e Mola nisaidie.

 

Green Ruwa

Mtoto wa Gwiji🇰🇪🇹🇿🇰🇪

greenruwa@gmail.com


Saturday, July 10, 2021

WAKUNYAKU

 




 

WAKUNYAKU



Mpole ukimuona, mwenye machache maneno,
Suti yake ya kushona, hakika haina mfano,
Warembo wakikutana, wamsema mkutano,
Jina lake Wakunyaku, yeyote ananyakua,

Amehama makanisa, hili sasa ni la saba,
Awamaliza vipusa, hata kwa zake hotuba,
Huyu ndugu anatesa, roho yake ya kahaba,
Jina lake Wakunyaku, yeyote anachukua,

Recho yule wa kwaya, Wakunyaku kamtwaa,
Siku hizi bila haya, wanatembea kwa mtaa,
Amtumia vibaya, na wala hatamuoa,
Jina lake Wakunyaku, yeyote anachukua,

Kuwawadia wageni, Wakunyakui namba wani,
Binti akiwa mgeni, ashamueka simuni,
Kesho yupo naye ndani, shamtoa kanisani,
Jina lake Wakunyaku, yeyote anachukua,

Yule mama wa fulani, aketiye katikati,
Walimuona njiani, na Wakunyaku wameketi,
Ni mama wa kanisani, na wanaitana switi,
Jina lake Wakunyaku, yeyote anachukua,

Kwenye maombi ya kesha, Wakunyaku hatakosa,
Anawatia puresha, wadada kwenye kanisa,
Anakitu chamuwasha, lazima tu atagusa,
Jina lake wakunyaku, yeyote ananyakua,

Kila kanisa nchini, halikosi Wakunyaku,
Iwapo hayupo ndani, basi yuko 'nje huku,
La, sio wewe jamani, naomba usijishuku,
Jina lake Wakunyaku, yeyote anachukua,

Sasa ni mda mwafaka, swala hili kuombea,
Tuliombee haraka, na pia kulikemea,
Tusije kuabika, kisa tumelipuzia,
Jina lake Wakunyaku, yeyote anachukua,


Green Ruwa
Mtoto wa Gwiji

Saturday, June 26, 2021

Chapati za kumi Nairobi


 CHAPATI ZA KUMI NAIROBI

    Nairobi, mji mkuu nchini Kenya wenye watu takriban milioni 4.397 ambao asili mia 60% ya wakaazi hao ni wafanya biashara. Uuzaji wa chapati Nairobi umekuwa ukinawiri kifaida ndani na nnje ya mji, ila kinachowapa  taabu wanunuzi ni ambapo chapati hizi zinapouuzwa bei ghali kinyume na matarajio yao.

                  Kutokana na utafiti wa matumizi ya ngano, imebainika wazi kwamba katika kila mwaka ngano hutumika kwa asii mia 47% ikilinganishwa na vyakula vyengine hata kwa jinsi bei ya vyakula vya ngano kama chapati kuuzwa bei ghali. 

                   Wanunuzi wengi wa chapati huwa vijana wanaofanya vibarua na wanabiashara wadogowadogo katika masoko na vituo vya mabasi, mara nyingi wateja wa chapati hupewa chakula hiki pamoja na mchuzi wa bure katika vibanda na hoteli nyingi zilizopo kando kando ya barabara na pia nnje ya maduka makbwa makubwa mjini Nairobi, 


                 Iwapo mtu angetaka chapti za shilingi kumi basi ni vyema kuwa tayari kuingia katika soko kubwa mjini  Nairobi, 'Muthurwa'. Katika soko hili chapati huuzwa kwa shilingi kumi, ni wachache wanaojua mahali ambapo chapati hizi za shiliingi kumi huuzwa. Julai 20.2021 niliweza kufika katika kibanda kimoja Muthurwa na kununua chapati ya shilingi kumi, hapa nilipakuliwa chapti hio kwa mchuzi wa maharagwe ambao uikuwa mchuzi wa bure. ''Hoteli hii hupata watu wasiopungua mia mbili kila siku'' alisema meneja wa hoteli hio. Kizuri zaidi katika hoteli hii ni kwamba mteja anaweza kulipa kupitia simu kwa mtandao wowoe ule.

            Magharibi mwa soko hili la Mudhurwa ndipo hoteli kama hii ya chapati za shilingi kumi na vyakula vyengine vitamu vya bei ya chini hupatikana. Mara kwa mara upande huu wa soko hupaswi kuamini watu hususan kwa barabara. Ni vizuri kuwa na ufahamu kamili wa pale unapoelekea katika soko hili maana vijana waliokaa kandokando ya njia hizi huwa na njama za kuwapora wapita njia pasi kutaka kujua wakati au masaa ya siku .

                 

Friday, June 25, 2021

ZINZI



 ZINZI


                  

Mara hii alirudi nyumbani akiwa mwenye huzuni, ‘’ wamekuchokoza tena?’’ aliuza bibi yake, Zinzi kwa unyonge akamkumbatia bibi yake anaemuona kama mama na baba katika maisha yake, mschana asiye na ugomvi akajiachilia kifuani mwa bibiye huku machozi yakimtoka kwa uchungu, kwa kigugumizi akajibu ‘’ndi-ndi-o bi-bi’. Zinzi mwenye umri wa miaka minane alikuwa amekerwa na kuchoka  na tabia za waschana wa shule ya mwembeni.

               Mschana kama zinzi wa darasa la nne hangeweza kujitetea anaposumbuliwa kwa maswali ya kejeli na wanafunzi waliomzidi umri na darasa, kwa hivyo alikuwa akinyamaza kama maji ya mtungini vijana wale walipokuwa wakimuuliza maswali kuhusiana na atokapo, iwapo amebeba vitabu au mawe begini na maswali mengine mengi ya kukera.

             Siku moja zinzi akiwa nyumbani, bibi yake alimuita na kumfunza kupiga mluzi kama firimbi ili kupata usaidizi kutokana na wale wanaomchokoza shuleni. Zinzi siku hiyo hakujuwa ni msaada gani atakaopata ila aliamua tu kumuamini bibi yake. 

             Ikatokea siku, zinzi akakutana na wanafunzi watano waliokuwa na sare chafu zilizojawa vumbi na viraka, ‘’mbona leo hujatubebea soda?’’ mmoja wao alimuuliza Zinzi,  kabla mwengine kufungua mdomo, Zinzi akapiga mluzi kwa nguvu, kukatokea njiwa wengi angani wakawanyeshea matone ya mavi na uchafu mwingi wanafunzi waliokuwa wakimchokoza Zinzi. Siku hiyo wanafunzi wale walipata aibu na kuchekelewa na wanafunzi wengine wote waliokuwa barabarani, zinzi alifurahi sana maana tangu siku hiyo wanafunzi wale wanapomuona humpisha na kunyamaza wasimuulize hata salamu. 

               

BINTI YETU

BINTI YETU Ni heri basi arudi, kuliko kututesea, Kwa sasa hatuna budi, sisi kama familia, Hizo dhiki zimezidi, mrudishe twakwambia, Binti ye...